Friday 20 March 2015

TFDA YATEKETEZA BIDHAA FEKI ZENYE THAMANI YA SH MIL.5, SIKONGE MKOANI TABORA


Baadhi ya bidhaa zilizoteketezwa na Maofisa wakaguzi wa TFDA wilayani Sikonge.
Maofisa wakaguzi wa TFDA kanda ya kati wakijiandaa kuteketeza bidhaa zilizoisha mda wake ikiwemo vinywaji wilayani Sikonge (picha na Allan Ntana).

Na Allan Ntana, Sikonge

MAMLAKA ya Chakula na Dawa (TFDA) Kanda ya Kati imefanikiwa kukamata na kuteketeza bidhaa mbalimbali za chakula, vinywaji, dawa za binadamu na mifugo, vipodozi na vifaa tiba vilivyoisha muda wake na vingine feki vyenye thamani ya zaidi ya sh mil.5 katika halmashauri ya wilaya ya Sikonge mkoani Tabora.

Akisoma taarifa ya ukaguzi mara baada ya kukamilika kwa zoezi hilo hapo juzi Afisa Mkaguzi wa Chakula Kanda ya Kati Sifa Chamgenzi alisema ukaguzi huo ulilenga kuangalia ubora na usalama wa dawa za binadamu na mifugo, uwepo wa vipodozi vilivyopigwa marufuku na bidhaa zingine zilizoisha muda wake wa matumizi. 

Alisema lengo la TFDA ni kufuatilia utekelezaji wa sheria na.1 ya mwaka 2003 ya chakula, dawa na vipodozi kwa wauzaji na wasindikaji wa vyakula na dawa na kuongeza kuwa zoezi hili lililenga kutekeleza mpango kazi wa Mamlaka hiyo wa kufuatilia ubora na usalama wa bidhaa hizo kwa mtumiaji.

Ukaguzi huo uliofanyika tarehe 20-29 Januari 2015 uliongozwa na Maafisa wakaguzi wawili kutoka TFDA Kanda ya Kati Fredrick Luyangi na Sifa Chamgenzi ambao waliungana na wakaguzi wenyeji wawili toka Ofisi ya Mkurugenzi Idara ya Afya na askari polisi wanne wilayani Sikonge na jumla ya majengo 118 yanayojihusisha na biashara ya chakula, vinywaji, dawa, vipodozi na vifaatiba yalikaguliwa.

Katika ukaguzi huo baadhi ya maduka yalikamatwa na vipodozi vilivyopigwa marufuku vikiwa na uzito wa kilo 164.4 na thamani ya sh 1,856,000/- na katika maduka ya vyakula walikamata vyakula vilivyoisha muda wake vyenye uzito wa kilo 825.5 vikiwa na thamani ya sh 2,720,000/-

Na katika maduka ya dawa za binadamu na mifugo walikamata jumla ya kilo 37 za dawa zilizoisha mda wake na feki zenye thamani ya sh 1,200,000/-.

Aidha katika ukaguzi huo kiasi cha sh 1,580,000 kilipatikana kutokana na ada za usajili wa maduka ya biashara ya chakula ambapo 40%  ya kiasi hicho sawa na sh 632,000 inabakia katika halmashauri kwa ajili ya kufanya kazi za TFDA.

Akizungumzia mambo waliyoyabaini wakati wa ukaguzi huo, Chamgenzi alisema ukaidi na uelewa mdogo wa sheria na.1 ya mwaka 2003 wa kulipa ada na tozo husika kwa baadhi ya wafanyabiashara wa maduka ya chakula, dawa na vipodozi bado ni tatizo sambamba na kutotoa ushirikiano kwa Afisa wakaguzi.

Aidha uwepo wa dawa bandia (feki) zilizoondolewa sokoni, dawa na vyakula vilivyoisha muda wake, kukosekana feni za kutunzia dawa katika stoo ya kituo cha afya Kitunda, maduka ya dawa za kilimo kuuza dawa za mifugo kinyume cha sheria, utunzaji mbovu na mlundikano wa dawa zilizoisha muda wake, viwanda na mashine za unga kuwa katika makazi ya watu ni miongoni mwa yaliyobainika.

Wakaguzi hao pia hawakuridhishwa na hali ya machinjio ya halmashauri hiyo kukosa uzio, kutokuwa na chanzo cha maji cha kuaminika na sakafu kuwa na mashimomashimo hali iliyosababisha kutuama kwa maji na damu na hivyo kuhatarisha afya za walaji, hivyo wakamwagiza mkurugenzi wa halmashauri hiyo Shadrack Mhagama kufanyia kazi mapungufu hayo kwani yanarekebika, jambo ambalo aliliafiki na kuahidi kutekeleza mara moja.

0 comments:

Post a Comment

NAIPENDA NCHI YANGU TANZANIA

Flag Counter

Text Widget